Mbowe ajibu hoja zilizoibuliwa na CCM
Wafuasi wa Chama Cha Mapinduzi, CCM, wakionyesha
bango lenye ujumbe wa amani na maendeleo yanayotokana na chama hicho cha
CCM, kwenye mkutano wa hadhara katika viwanja vya Jangwani jijini Dar
es Salaam jana.
Ikiwa ni wiki mbili baada ya Chadema
kutoka mashambulizi kwa serikali, mawaziri hao wamejitokeza kujibu
mapigo katika mkutano wa hadhara ulioandaliwa na CCM kwenye viwanja vya
Jangwani jijini Dar es Salaam, eneo ambalo Chadema walilitumia kurusha
mashambulizi hayo na kuzindua mpango wao ujulikanao kama Movement for
change (M4C).
Akizungumza kwenye mkutano huo, Waziri wa
Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, alisema moja ya kero inayolikabili
jiji la Dar es Salaam ni jeuri ya baadhi ya wamiliki na wafanyakazi wa
daladala ambao hupandisha nauli bila kufuata utaratibu uliowekwa na
serikali.
Dk. Mwakyembe alisema wiki mbili
zilizopita, taasisi iliyo chini ya wizara yake, Mamlaka ya Udhibiti wa
Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (Sumatra) walikamata daladala 19 kwa
kuongeza nauli kinyume cha sheria.
“Katika kujiridhisha nikasema siwezi
kwenda Bungeni nikaacha hali ya Dar es Salaam ni mbaya kwa upande wa
nauli, nikapanda daladala kutoka Mwenge kwenda Tegeta na Tegeta kwenda
Bunju, badala ya nauli ya Sh. 500 kutoka Mwenge kwenda Tegeta nikatozwa
Sh. 1000, kutoka Tegeta mpaka Bunju nilitozwa sh. 1,500, huku ni
kuwaumiza wananchi na kuchezea sheria za nchi,” alisema Dk. Mwakyembe.
Alisema watu wanapandisha nauli utadhani
wizara yake haipo, na kuahidi kuwashukia wamiliki wa daladala na kwamba
watakosa mahali pa kukimbilia na atalazimika kuchelewa kwenda bungeni
ili kuhakikisha kero hii inapatiwa ufumbuzi haraka.
Waziri Mwakyembe alisema hakuna sababu ya
watu kupandisha nauli ovyo ovyo kama vile serikali imekwenda likizo
wakati upo utaratibu wa kisheria wa kufanya hivyo.
“Na sio huko tu kwenye daladala na wengine
wote wanaopandisha nauli ovyo kwa kisingizio cha gharama zimepanda,
kuna utaratibu wa kisheria kupandisha gharama, kama una maombi yako
peleka Sumatra, Sumatra wataitisha mkutano wa wadau, watajadiliana
itarudi kwetu, tutaliangalia kama kweli gharama zimepanda halafu tutatoa
bei elekezi, sio kila mtu kujiamulia tu, hii ni serikali,” alisema Dk.
Mwakyemba.
Dk. Mwakyembe ambaye alikuwa kivutio
kwenye mkutano huo kutokana na msimamo wake, alitumia fursa hiyo kutoa
namba yake ya simu ya mkononi ya 0782 242526 akiwataka wananchi
wampigie wakati wowote wanapoona daladala inawadhulumu kwa kuwatoza
nauli kubwa ambayo haipo kisheria.
Akizungumzia tatizo la msongamano wa
magari katika jiji la Dar es Salaam, alisema foleni zilizopo kimsingi
zinaua uchumi wa nchi hasa ikizingatiwa kwamba mkoa wa Dar es Salaam
ndio tegemeo la kiuchumi nchini.
Alisema katika kukabiliana na kero hiyo,
wizara yake imejipanga katika mwezi mmoja ujao kuanzisha usafiri wa
treni wa Tazara kutoka Mwakanga hadi Kurasini kila asubuhi na kutoka
Ubungo Maziwa hadi Stesheni, ambapo wataalamu wake wamemuambia huduma
hizo zitabeba zaidi ya abiria 9,600 kwa mkupuo.
Aidha alisema wakati anaingia wizarani
alikuta wawekezaji wanaotaka kuendesha huduma ya treni, lakini amewapiga
‘stop’ na kwamba kazi hiyo itafanywa na Watanzania wenyewe kupitia
serikali yao.
Kuhusu Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA),
alisema haja ridhika kabisa na utendaji kazi wa mamlaka hiyo na amewapa
muda wajiandae kabla hajafanya ziara rasmi kwani anazo taarifa kuwa
wafanyakazi wake wamegeuka wafanyakazi wa ‘super market’ ya kuuza 'spare
parts' ya magari kutoka nje.
Dk.Mwakyembe alisema watendaji wote
wanaofanya biashara hiyo atawashughulikia kwa kuwang’oa hata kama
wanajiona ni wakubwa kuliko mti wa Mbuyu.
“Nawakumbusha wenzangu wa bandari ya Dar
es Salaam ambayo inatakiwa kuwa sifa na kioo cha Tanzania, mimi
sijaridhika nayo kabisa na nimefanya makusudi sijaenda kuwatembelea
pale, nataka wajipange sawasawa wasije wakanilaumu mbele ya safari,”
alisema huku akishangiliwa na umati wa mashabiki na wanachama wa CCM.
Alisema Tanzania haiwezi kuwa nchi
iliyopewa fursa na Mungu kuweza kuwa na lango kuu la nchi sita
zinazohitaji huduma hapa lakini nchi hizo zinaikimbia Tanzania kwa
sababu ya upuuzi unaofanywa na baadhi ya watendaji wa bandari hiyo.
Dk.Mwakyembe aliwaomba wananchi katika
kipindi atakachokuwa katika wizara hiyo hatua atakazokuwa anazichukua
dhidi ya watendaji wasiowaaminifu wasiwe wanalalamika na kwamba atatumia
miezi mitatu kusafisha uozo uliopo katika wizara na taasisi zake.
Naye Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais,
Mahusiano na Uratibu, Steven Wasira, alianza kwa kuwashangaa watu
wanaosema kuwa serikali ya CCM haijafanya kitu kwa Watanzania tangu
wakati wa uhuru.
Alisema suala la kupanda kwa bei za vitu
kama mafuta, si la CCM kwani linaanzia nchi za Uarabuni ambako mafuta
hutoka huko na kulifanya tatizo hilo la kidunia zaidi.
“Wapo watu wanasema hili tatizo la ugumu
wa maisha ndiyo sera ya CCM lakini tujiulize kwani mafuta yakipanda bei
Uarabuni, je! CCM iko Uarabuni? Alihoji Wasira na kuongeza kuwa serikali
imekuwa ikichukua hatua mbalimbali katika kukabiliana na hali hiyo.
Alisema wanaolalamikia suala la ugumu wa
maisha ni kwasababu tu hawajui kwani Tanzania huwezi ukalinganisha na
nchi ambazo zipo katika kundi la G8 ambazo uchumi wake upo juu.
Wasira alisema hata hivyo zipo hatua
kadhaa zinazochukuliwa na serikali ambapo miongoni mwa hatua hizo ni
kuwekeza kwenye kilimo cha mabonde ya Kilombero ambako hekta 100,000
zimetengwa kwa ajili ya kilimo cha mpunga.
Kuhusu kukabiliana na tatizo la kupanda
kwa bei ya sukari nchini, alisema katika bajeti ya mwaka huu serikalini
imeainisha mabonde ya Kilombero, Rufiji, Wami, Maragarasi na Kagera kwa
ajili ya kujenga viwanda vya kuzalisha sukari.
Tatizo la kupanda kwa gharama za umeme,
Waziri huyo alisema kuanzia mwezi Julai mwaka huu kutajengwa bomba la
gesi kutoka Mtwara hadi Dare s Salaam ambapo gesi hiyo itatumika kwa
ajili ya kuzalisha umeme na hivyo kupunguza gharama ya nishati hiyo
kutoka dola senti 42 hadi kufikia dola senti saba za Marekani.
Alisema watu wanaosema kuwa serikali ya CCM haiwajali wananchi wake na haina lolote inachowafanyia, ni sawa na kufuru.
“Nataka kumpa ujumbe Mbowe (Mwenyekiti wa
Chadema) anapo sema hatujafanya lolote anamkufuru baba yake mzazi
aliyedai uhuru na Mwalimu Nyerere, namsihi asije akapata laana kwa kauli
zake hizo,” alisema Waziri.
Kwa upande wake, Waziri wa Ardhi, Nyumba
na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka, alikiri kuwepo kwa kero
nyingi kwenye sekta ya ardhi na kwamba ufumbuzi wa kero hizo umekuwa
ukifanywa kwa kuzingatia sheria za nchi zilizopo.
“Katika sekta ya ardhi tunakwenda kwa
sheria, na wahahkikishia wananchi hakuna mtu yoyote atakayeporwa ardhi
yake bila kulipwa haki yake,” alisema
Profesa Tibaijuka alisema wananchi ambao
waliporwa ardhi zao kwa ubabe aidha na watendaji wa kata au vijiji,
wapeleke kero hizo ofisini kwake ili aweze kuzifanyia kazi haraka
iwezekanavyo.
Naye Wziri wa Maji, Profesa Jumanne
Maghembe, alisema wizara yake imejipanga kutatua kero za maji katika
jiji la dare s Salaam na maeneo mengine kama Ilani ya CCM inavyoelekeza
ifikapo mwaka 2015 upatikanaji wa maji mijini ifikie asilimia 90 kutoka
asilimia 65 za sasa na vijijini kutoka asilimia 50 hadi asilimia 65.
Kuhusu upanuzi wa mtambo wa Ruvu Chini,
alisema kuwa wanaupanua kutoka chujio moja hadi matano ambapo gharama
zake zitakuwa ni dola milioni 37 na ujenzi huo unatarajiwa kukamilika
Machi mwakani hali kadjhalika na ule wa Ruvu Juu.
Alisema katika mwaka wa fedha 2012/13
serikali imetenga sh. bilioni 16 kujenga bomba kubwa lenye upana wa mita
1.8 umbali wa kilomita 58 kutoka Ruvu Chini hadi matenki ya yaliyopo
Chuo Kikuu cha dare s Salaam.
Profesa Maghembe alisema katika mwaka huu
wa fedha serikali imetenga sh. bilioni 15 kujenga visima eneo la Kimbiji
na Nampera hali kadhalika inatarajia kujenga bwawa kubwa la Kidunga
mkoani Morogoro lengo likiwa ni kuongeza upatikanaji wa maji katika jiji
la dare s Salaam.
Naye Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli,
alisema kuwa nchi nzima kuna miradi ya barabara yenye urefu wa kilomita
11,154 inayoendelea kujengwa kwa kiwango cha lami na kwamba otakapo
kamilika hata Chadema wataendeleza maandamano yao kupitia barabara za
lami.
Alisema miradi yote hiyo inagharimu kiasi cha shilingi trilioni sita ambapo nusu yake zimetolewa na serikali ya Tanzania.
“Nawapongeza wapinzani, waendelee
kuandamana katika barabara za lami maana natambua kuwa shukurani ya
punda ni mateke, na wasione vyaelea vimeundwa, pia unaweza kumbeba mtu
mgongoni kumvusha mtoni na unapofika ng’ambo na kumshusha anakuambia
kwanza mgongo wake ulikuwa unanuka,” alisema.
MBOWE AJIBU MAPIGO
Chama cha Demokrasia na Maendeleo
(Chadema) kimejibu baadhi ya hoja zilizoibuliwa na Chama Cha Mapinduzi
(CCM) kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika jana kwenye viwanja vya
Jangwani jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti na Katibu Mkuu wa Chadema,
Freeman Mbowe na Dk Wilbrod Slaa, walitoa majawabu hayo wakati
wakihutubia kwenye mkutano wa hadhara wa Operesheni Okoa Kusini
uliofanyika jana kwenye uwanja wa Likangara mjini Ruangwa, mkoa wa
Lindi.
Dk Slaa alisema kilichofanywa na mawaziri
wa serikali ya CCM ni kutoa maneno yasiyolingana na uhalisia wa mambo
yalivyo ndani ya jamii.
“Viongozi waliopo serikalini hawana wajibu
wa kupiga maneno, wanatoa kauli zisizolingana na uhalisia wa hali
ilivyo, wanachotakiwa kukifanya ni kufanya kwa vitendo ili matokeo yake
yaonekane kwa umma,” alisema.
Pia Dk Slaa alisema sehemu kubwa ya hotuba
za mawaziri hao zililenga katika ‘tutafanya’, hali iliyoonyesha kuwa ni
ahadi zilizotolewa miaka mingi pasipo utekelezaji.
Dk Slaa alisema mafanikio yalitajwa na
mawaziri wa CCM kwenye mkutano huo, ni sehemu ndogo ya matokeo
yaliyopaswa kuonekana, hasa kutokana na rasilimali zilizopo nchini.
“Mafanikio wanayoyataja ni mfano wa punje tu, sehemu kubwa ya pato la nchi hii linaliwa na watu wachache,” alisema.
Dk Slaa alisema kama fedha zilizoibwa na
mafisadi zingenusuriwa na kurejeshwa kwa ajili ya uboreshaji wa
maendeleo na ustawi wa jamii, mafanikio yangepatikana zaidi ya
yaliyotajwa na mawaziri wa serikali ya CCM.
Kwa upande wake, Mbowe alisema kauli
iliyotolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Uhusiano wa Jamii), Steven
Wassira, kuhusu uhusiano wa Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere
na marehemu Elikaeli Mbowe (baba yake mzazi), ililenga kuupotosha umma.
“Mzee Mbowe alikuwa na uhusiano na Mwalimu
Nyerere katika kutetea haki na kuingiza damu ya Utanzania ndani ya
mioyo ya wananchi, sina haja ya kumjibu sana Wassira lakini ajue kwamba
waliopo sasa ndani ya CCM wanaendeleza maslahi binafsi tu,” alisema.
Alithibitisha marehemu Mbowe kushiriki
harakati zilizoongozwa na Mwalimu Nyerere, lakini akasema uhusiano wao
ulilenga kuitumikia jamii na si kuiba na kupora rasilimali za umma.
Alitoa mfano kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya
Korosho ni Anna Abdallah ambaye ni mke wa Makamu Mwenyekiti wa CCM, Pius
Msekwa na Mbunge wa zamani wa Lulindi, lakini ameshindwa kusaidia kero
zinazowakabili wakulima wa korosho.